Taarifa ya utekelezaji wa ilani ya chama cha Mapinduzi katika Jimbo La Maswa Magharibi


HALMASHAURI YA WILAYA YA MASWA
OFISI YA MBUNGE - JIMBO LA MASWA MAGHARIBI
MKOA WA SIMIYU.
TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA 
ILANI YA CHAMA CHA MAPINDUZI
KATIKA JIMBO LA MASWA MAGHARIBI,
2015/2016 - 2019/2020.




1.       ELIMU.
Katika kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa sekta ya elimu, Jimbo ilijiwekea malengo ya kuhakikisha kuwa vijiji vyote vilivyoko jimboni vinakuwa na shule ya msingi ili kuhakikisha kuwa watoto wote waliofikisha umri wa kwenda shule wanaandikishwa. Lengo linguine lilikuwa kuhakikisha kwamba kata zote zinakuwa na shule ya sekondari ili kuwezesha watoto wote wanaofaulu wanajiunga na masomo ya  sekondari.

Inaendelea ...........


Utekelezaji:

Elimu ya Msingi. Mbunge alishiriki kikamilifu katika uhamasishaji wananchi kuchangia nguvu, muda na raslimali pesa ili kujenga madarasa katika vijiji 3 vya Ngazu, Mwakulilima na Ng’hungu. Hivi ni vijiji vilivyokuwa havina shule za msingi kabisa. Watoto walikuwa wanatembea umbali mrefu kwenda kwenye shule zilizoko vijiji vingine. Jumla ya madarasa 8 yamejengwa, madarasa 4 kila kijiji yamejengwa na shule kufunguliwa katika kijiji cha Ngazu na kijiji cha Mwakulilima. Madarasa 2 na ofisi ya mwalimu yamekwisha kujengwa katika kijiji cha Ng’hungu na shule itafunguliwa baada ya choo cha shule kukamilika.


                Mwonekano wa baadhi ya madarasa ya shule ya msingi Ngazu.

Kwa sababu ya ongezeko la watoto walioandikishwa kujiunga na madarasa ya awali na shule za msingi mwaka 2016, na kwa kuwa utekelezaji wa sera ya elimu bila malipo sera inayotekelezwa na serikali ya awamu ya tano ulihamasisha wazazi kuwapeleka watotowao shuleni, uandikishaji katika shule za msingi uliongezeka Zaidi na matokeo yake watoto wengi walikosa madarasa ya kusomea. Kwa kushirikiana na halmashauri ya wilaya, mbunge alihamasisha ujengaji wa madarasa jimboni ambapo kila kijiji kiliweza kujenga boma moja la darasa na mbunge kupitia mfuko wa jimbo alitoa bati 40 kila shule ya msingi ili kuezeka madarasa hayo. Jumla ya madarasa 58 yaliezekwa kupitia mpango huo kwa maana ya darasa moja kila kijiji chenye shule ya msingi.

Ili kuhakikisha miundo mbinu ya shule inatosheleza mahitaji ya wanafunzi, mbunge alitoa kutoka mfukoni mwake pesa yenye kutosheleza mbao zenye kutosheleza kuezeka madarasa 3 na ofisi 1 (Thamani ya Tshs 3,388,000/=) katika shule ya msingi ya kijiji cha Zawa. Shule hii ina wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la saba, lakini ilikuwa na vyumba 4 tu vya madarasa, hivyo kulazimika wanafunzi wa madarasa mengine kusomea darasa moja kwa mtindo wa mzungu wa nne (mzungu four).

Katika kuhamasisha na kuwatia hamasa walimu wa shule za msingi walioshika namba kumi bora katika wilaya kwa matokeo ya mitihani ya darasa la saba mwaka 2016, mbunge alitembelea shule zote kumi zilizofanya vizuri na kuwapa zawadi ya mipira 2 (wa miguu na pete) kila shule na kuwapatia walimu Tshs laki moja (100,000/=)  kwa kila shule iliyofanya vizuri kama motisha kwa walimu kwa kusaidia watoto kufanya vizuri katika masomo yao. Mpango huu wa kuhamasisha walimu kufundisha kwa bidi unaendelea ambapo mheshimiwa mbunge aliahidi na kutoa Tshs 50,000 kwa kila mwalimu wa sekondari ambaye somo lake litapata A katika mtihani wa taifa kwa mwaka 2018.  Pia mbunge ameahidi kuwapatia Tshs laki moja kila shule ya msingi itakayokuwa miongoni mwa shule kumi bora ki wilaya.


             Zawadi ya mipira na jezi kwa shule ya msingi Igwata ilikuwa miongoni mwa shule kumi bora kiwilaya.
   
Kwa upande wa elimu ya sekondari, tumewezesha kwa mara ya kwanza katika jimbo,  kuwa na sekondari ya kidato cha tano na sita (Malampaka High School) kuanzia mwaka 2016. Tulifanya mawasiliano na wizara ya elimu kupitia waziri wa elimu profesa Ndalichako na kukubali kutupatia pesa ili kujenga bwalo la chakula, kujenga mabweni 2, kumalizia mabweni 2 yaliyokuwa hayakukamilika, kuweka umeme, na kuchimba kisima cha maji. Sasa hivi tayari shule ina kidato cha tano na sita.

Ili kuwasaidia watoto wa kike kuwaepusha na kutembea umbali mrefu, tumejenga bweni moja la kukaa wasichana katika shule ya Sekondari Badi na kusaidia gharama za uwekaji wa umeme shuleni hapo. Ofisi ya mbunge ilitoa wazo la kuanza ujenzi wa bweni na kuchangia mifuko 200 ya simenti ili kuanza ujenzi. Wananchi wa kata ya Badi walitoa mchanga, mawe na fedha kwa ajili ya kumlipa fundi ili kujenga boma. Baada ya hapo mbunge aliwaomba Shirika lisilo la kiserikali la World Vision kusaidia upauaji na kumalizia hatua zote zilizokuwa zimebaki. Ombi hilo lilikubaliwa. Kwa niaba ya wananchi tunawashukuru sana Shirika la World Vision kwani wamekuwa waungaji mkono wakubwa kwa maendeleo ya jimbo. Bwalo limekamilika na linatumika kwa sasa.


Mbunge (Mashimba Ndaki) akishiriki ujenzi wa bweni la wasichana – Badi sekondari.

Kwa kusaidiana na benki ya NMB tumewezesha kuezeka madarasa 2 na ofisi shule ya sekondari Mataba. NMB walitoa mabati na mbunge akatoa simenti mifuko 100 ya kumalizia kuweka lenta, kupiga lipu na kununua mbao zote za kuezekea. Jumla ya gharama zilizotolewa na mbunge ni Tshs ……..kutoka katika mfuko wa jimbo.

Kati ya kata 17 zilizoko kwenye jimbo la Maswa Magharibi, Kata 2 hazina sekondari za kata,  nazo ni kata za Zanzui na kata ya Mwang’honoli. Mbunge kwa kushirikiana na wananchi wa kata hizo wameanzisha ujenzi wa shule za sekondari na mpaka sasa hivi kuna maboma ya madarsa manne na ofisi 2 katika kata ya Zanzui. Madarasa 2 na ofisi 1 tayari yameezekwa. Mbunge alitoa mabati 240 yenye thamani ya Tshs 6,000,000 kutoka mfuko wa jimbo. Katika kata ya Mwang’honoli tayari madarasa 2 na ofisi yameshajengwa na kuezekwa. Mbunge alitoa fedha za mfuko wa jimbo Tshs 1,495,000 ili kusaidia uezekaji.

Katika juhudi za kutaka kuwa na makazi bora kwa walimu wa shule za sekondari, serikali ilitoa Tshs 150,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba 6 za walimu shule ya sekondari ya Mwabayanda. Hii ilikuwa ni juhudi za mbunge baada ya kuzungumza na uongozi wa wizara ya elimu juu ya umuhimu wa shule hii kuwa na makazi ya walimu kwa kuwa iko maeneo ya pembezoni sana.

Elimu ya ufundi ni muhimu sana hasa wakati huu ambapo vijana wengi wanamaliza darasa la saba na sekondari lakini hawachaguliwi kuendelea na masomo ya elimu ya  juu. Kwa kulitambua hilo mbunge kwa kushirikiana na halmashauri ya wilaya walipeleka maombi ya kuboresha chuo cha maendeleo ya wananchi Malampaka na serikali imetoa fedha kiasi cha Tshs 590,000,000 ili kujenga majengo mapya ikiwemo mabwalo ya wasichana na wavulana, kuongeza madarasa na kujenga karakana moja. Baada ya kukamilika uboreshaji huu, chuo kitakuwa na uwezo wa kudahiri wanafunzi wengi Zaidi na hivyo kusaidia vijana wengi kupata ujuzi ili wajiajiri wenyewe.

Ufaulu mkubwa wa wanafunzi wa darasa la saba mwaka 2018 ulisababisha miundo mbinu ya madarasa katika shule za sekondari kuzidiwa na kusababisha baadhi ya wananfunzi waliochaguliwa kuanza kidato cha kwanza mwaka 2019 wasianze masomo kwa sababu ya upungufu mkubwa wa vyumba vya kusomea. Mbunge kwa kusaidiana na halmashauri ya wilaya alihamasisha wananchi katika jimbo kujenga na kumaliza boma la darasa moja kila shule ya sekondari katika sekondari zote 17 zilizoko jimboni. Katika jitihada hizo serikali ilitoa Tshs 150,000,000 ili kuunga mkono juhudi za wananchi katika kuhakikisha kuwa madarasa yaliyopungua yanakamilika na kuanza kutumika ili watoto waliochaguliwa lakini hawakujiunga na kidato cha kwanza kwa sababu ya upungufu wa madarasa waende shule. Shule za sekondari 7 zilipata msaada huo wa serikali.

Ili kuwezesha kuinua taaluma katika shule zetu, ofisi ya mbunge kupitia mfuko wa jimbo iiwezesha upatikanaji wa mashine ya kudurufu mitihani (photocopier machine). Mashine hii imesaidia kudurufu mitihani ya wilaya na kimkoa na kurahisisha ufanyaji wa mitihani kwa wanafunzi.

2.      AFYA: Ili kutekeleza Ilani ya CCM jimboni kwa upande wa sekta ya afya, lengo kuu lilikuwa kuboresha huduma za afya jimboni kwa wananchi wote hususani wanawake na watoto.

     Utekelezaji:

Uboreshaji wa kituo cha afya Malampaka umekamilika. Serikali ilitoa milioni 500 ili kukiboresha kituo hiki na kazi zifuatazo zimekamilika: Jengo la upasuaji limekamilika. Jengo la wodi ya kawaida limekamilika. Chumba cha maabara kimekamilika. Jengo la nyumba ya mtumishi limekamilika. Jengo la kuhifadhia maiti nalo limekamilika. Kukamilika kwa uboreshaji wa kituo hiki utapunguza kwa kiasi kikubwa vifo vinavyotokana na uzazi kwa wanawake lakini pia kupata huduma za upasuaji karibu badala ya kusafiri umbali mrefu.

Mbunge (wa tatu kutoka kulia) akiwa na baadhi ya viongozi na wananchi walipotembelea kituo cha afya Malampaka.

Ujenzi wa kituo cha afya cha Mwabayanda unaendelea vizuri. Hii ni baada ya serikali kutoa kiasi cha Tshs milioni 400. Majengo yanayoendelea kujengwa katika kituo hiki cha afya ni pamoja na jingo la wodi ya akina mama, jingo la upasuaji, jingo la maabara, nyumba ya mtumishi, jingo la maabara na jingo la kuhifadhia maiti. Kituo hiki kitakapokamilika kitahudumia wananchi wa kata za Mwabayanda, mwang’honoli, Kulimi na baadhi ya vijiji vya kata ya Busangi na Nyabubinza.


Ujenzi wa kituo cha afya cha kata ya Mwabayanda uko katika hatua za mwisho kukamilika.

Katika azima ya kuwasaidia akina mama jimbo pia lilipata ufadhili wa shirika la AMREF kwa kujenga wodi za akina mama katika zahanati za Masela, Mwabagalu, na Jija. Pamoja na wodi hizo, shirika pia linasaidia kujenga vituo vya kuelimisha vijana katika zahanati hizo ili vijana wawe wanaelimishwa kuhusu mambo yanayohusu uzazi salama. Wodi nyingine ya wazazi iliyojengwa ni ile ya zahanati ya Badi ambapo serikali kwa kushirikiana na UNFPA wamewezesha kukamilika kwa jingo hilo.

Kwa kutumia mfuko wa jimbo na michango ya wananchi, mbunge amewezesha kuezekwa kwa maboma 8 ya zahanati katika vijiji vya Kizungu, Mwang’anda, Mwatumbe, Nyabubinza, Bukangilija, Jihu,  Isulilo na Wigelekelo. Mbunge kwa kushirikiana na Halmashauri ya wilaya aliomba Shirika la World Vision kumalizia zahanati za Mwatumbe na Wigelekelo, Shirika hilo lilikubali na tayari linamalizia ujenzi wa zahanati hizo 2. Mbunge pia amepeleka maombi kwa shirika hilo ili kumalizia zahanati za Mwang’anda na Jihu mwaka ujao wa fedha.

Kwa msukumo wa mbunge pia kupitia mfuko wa jimbo, serikali kwa kusaidiana na wananchi tumewezesha kumalizia ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Kidabu, zahanati iliyojengwa boma lake muda mrefu lakini haikukamilika. Sasa hivi wananchi tayari wanapata huduma kwenye zahanati hii baada ya kuimalizia. Kwa mtindo huo huo wa kusaidiana na wananchi, mbunge na serikali, tumeweza kujenga jengo la wagonjwa katika zahanati ya kijiji cha Igunya na tayari jengo hilo lilishakamilika na  linatumika.

Kwa kutumia mfuko binafsi na kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo mbunge, aliweza kutoa magodoro 10 kwenye kituo cha afya cha Malampaka na kutoa vifaa vya kutumia wakati mama anajifungua na baada ya kujifungua (birthing kits) kwa zahanati za Badi, Masela, Seng’wa na kituo cha afya cha Mwasayi. Aidha, ofisi ya mbunge ilichangia kwa sehemu kubwa kupitia mfuko binafsi wa mbunge ujenzi wa vyoo vya wanafunzi vya shule ya msing Sayusayu, shule za sekondari Mataba, na Mwabayanda.

3.      MAJI
Lengo kuu katika sekta hii ya maji lilikuwa kuwapatia maji safi na salama wananchi wa jimbo la Maswa Magharibi na kuhakikisha kwamba akina wametua ndoo kichwani.

Utekelezaji:

Mradi mkubwa wa maji umeanzishwa Kata ya Mwang’honoli. Mradi huu uko katika vijiji viwili vya Mwabulimbu na Ngazu. Hatua iliyofikiwa ni uwekaji wa mashine ya kusukuma maji, ulazaji wa mabomba na ujenzi wa vituo vya kuchotea maji (water points). Kwa sasa mradi uko katika hatua za mwisho za majaribio kupeleka maji katika vijiji vya Mwabulimbu na Ngazu. Mradi huu ni matokeo ya juhudi za mbunge wa jimbo kufuatilia upatikanaji wa fedha kwani kisima kinachotumika kutoa maji kilichimbwa zamani lakini fedha za ujenzi wa mtandao wa maji ikiwa ni pamoja na kuweka mashine ya kusukuma maji hazikupatikana. Tunaishukuru sana serikali ya awamu ya tano chini ya Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kutupatia fedha taslimu kiasi cha Tshs milioni 500 za kukamilisha mradi huu.

Katika kata ya Badi kuna miradi miwili ya maji ya kupeleka maji katika vijiji vya Jihu, Ikungu, Nyashimba na Muhida.. Mradi huu utakuwa na mashine 2 za kusukuma maji, moja itasukuma maji kupeleka vijiji vya Jihu na Ikungu na nyingine itasukuma maji kupeleka vijiji vya Nyashimba na Muhida. Mpaka sasa hivi majengo ya pampu yote mawili yameshakamilika, ulazaji wa mabomba kwenda vijiji vya Jihu na Ikungu umekamilika, vituo vya kuchotea maji vyote vimeshajengwa na ujenzi wa matanki unaendelea vizuri. Mradi utakapokamilika utawasaidia wananchi wa vijiji vinne kuwa na maji safi na salama.

Kwa kushirikiana na shirika la World Vision, mradi wa kisima kirefu ulichimbwa katika kijiji cha Isulilo na kuwezesha kupatikana maji mengi ya kutosheleza wakazi wa kijiji hicho. Mheshimiwa mbunge amewaomba Shirika hilo kusaidia kuweka mashine ya kusukuma maji ili maji ya kisima kilichochimbwa yaweze kuwafikia watu wengi. Shirika limekubali na kazi ya kuchimba mitaro inaendelea kufanywa na wananchi. Mradi huu utakapokamilika utakuwa na vituo 6 vya kuchotea maji kwenye kila kitongoji cha kijiji cha Isulilo.

Katika kata ya Jija, kabla ya kuchaguliwa kuwa mbunge kulikuwa na mradi wa maji uliokuwa umekwama kwa muda wa miaka 3. Mradi huu ulikosa ufuatiliaji hali iliyopelekea mradi kutokamilika kwa wakati. Kwa ufuatiliaji wa mbunge, mradi ulitekelezwa na kukamilika mwaka 2017.

Mradi wa Sayusayu extension unaokusudia kupeleka maji kijiji cha Ng’haya uko kwenye hatua nzuri ya kukamilika. Kazi ya kujenga vituo vya kuchotea maji imekalika na ulazaji wa mabomba unaendelea vizuri. Mradi utakapokamilika utawasaidia sana wananchi wa kijiji cha Ng’haya kwa kuwa hupata maji kutoka umbali mrefu.

4.      BARABARA/RELI NA UMEME:


Katika kipindi tajwa miundo mbinu ya barabara na umeme imeimarishwa na mingine kujengwa upya. Wakati awamu ya tano inaanza kulikuwa na vijiji 14 ambavyo havikuwa na umeme katika jimbo. Mpaka wakati wa kuandika taarifa hii vijiji 4 tayari vimeshafikiwa na umeme wa REA, ambavyo ni Inenwa, Nhelela, Gumali, na Kakola. Bado vijiji 10 havina umeme.

Kuhusu barabara, Jimbo limeweza kufunguliwa kwa barabara zinazounganisha vijiji na vijiji. Barabara kutoka kijiji cha Gulung’washi kata ya Malampaka kwenda Kata ya Kadoto kupitia Mwabulimbu, Mwang’honoli, na Zawa imelimwa kwa kiwango cha changalawe. Barabara hii itaiwezesha kata ya Kadoto na Mwang’honoli kupata huduma yake kwa urahisi kutoka mji mdogo wa Malampaka na hivyo kuchagiza shughuli za kiuchumi za wananchi wa maeneo hayo. Barabara ya kuunganisha kijiji cha Jihu na Ikungu imelimwa ili kufanya kijiji cha Ikungu kuunganishwa na vijiji vya Muhida na Malampaka. Barabara ya kutoka Kulimi kuunganisha vijiji vya Mwamihanza na Ngongwa inafanyiwa matengenezo pia.

Kwa upande wa reli, tunaishukuru sana serikali ya awamu ya tano chini ya Mheshimiwa Rais Dr. John Pombe Joseph Magufuli kwa ujenzi wa reli ya kisasa. Reli hii inapita katika jimbo letu na matarajio yetu ni kwamba mipango ya kujenga bandari kavu katika kituo cha Malampaka itaendelea sambamba na ujenzi wa reli hiyo. Kwa upande wa jimbo tayari tumeiomba halmashauri ya wilaya kupima viwanja katika mji mdogo wa Malampaka na tayari wilaya imetekeleza hilo. Kwa sasa tayari kuna viwanja vya kujenga maghala, makazi, nyumba za kulala wageni na mahotel. Tunaendelea kuhamasisha wananchi wa ndani ya jimbo, wilaya, mkoa na kwingineko wajitokeze kujenga ili reli itakapokamilika kila kitu kiwepo ikiwa ni pamoja na mahali pa kuhifadhi bidhaa mbalimbali zitakazokuwa zikishushwa bandari kavu ya Malampaka.

Madaraja na vivuko mbalimbali yamejengwa ikiwa ni pamoja na daraja la Kinamwigulu ambalo lilikuwa limekatika muda mrefu na hivyo kusababisha vijiji vingi kutengwa na makao makuu ya wilaya. Sasa hivi daraja hilo limekamilika na wananchi wanapita kwa urahisi wanapofanya shughuli zao za kiuchumi. Barabara kuunganisha kata ya Zanzui na kata ya Mwamashimba ilifanyiwa matengenezo na kuweka vivuko kati ya kijiji cha Zanzui na Dodoma kuwezesha kupitika wakati wote wa mvua na masika.

Mheshimiwa mbunge anaishukuru sana serikali kwa niaba ya wananchi wa jimbo kwa kuunganisha mkoa wa Simiyu na Shinyanga kupitia jimbo la Maswa Magharibi. Barabara ya Mwigumbi mpaka Maswa kwa sasa tayari imekamilika kujengwa kwa kiwango cha lami. Faida za barabara hii pamoja na kuunganisha mkoa na mikoa mingine, lakini pia wananchi wa jimbo la Maswa Magharibi wataweza kupata masoko ya mazao yao na huduma zingine kwa urahisi Zaidi kwa sasa kulinganisha na huko nyuma. Mbunge wa jimbo anayo matumaini makubwa kwamba barabara ya kutoka Ikungu/Njiapanda kwenda Malampaka pia itamalizika kujengwa kwa wakati kwa kiwango cha lami kwa sababu tayari mwaka wa fedha 2018/2019 ilipangiwa bajeti ya Tshs milioni 800 na mwaka huu wa fedha 2019/2020 pia imepangiwa bajeti ya Tshs milioni 300. Tayari mkandarasi wa kujenga barabara hii ameshaanza kazi ya ujenzi.

5.      KILIMO NA UZALISHAJI:

Pamoja na kuisimamia serikali ngazi ya wilaya mpaka taifa, ofisi ya mbunge imeweza pia kuhamasisha wakulima ndani ya jimbo kulima na kuzalisha mazao kwa tija kubwa ili kujipatia mazao mengi na hivyo kujiongezea kipato hatimaye. Kwa kushirikiana na tume ya umwagiliaji ya kanda na wilaya mradi wa mtaro wa umwagiliaji wa Kinamwigulu umekamilika. Mheshimiwa mbunge kwa kushirikiana na Shirika la World Vision waliweza kukamilisha mradi wa umwagiliaji wa Masela kwenye kitongoji cha Isebya. Vijana wa kikundi cha kijiji cha Gumali walipatiwa msaada wa pampu ya umwagiliaji na mifuko 10 ya siment ili waweze kukarabati mtaro wao wa maji unaotumika kupeleka maji kwenye majaruba ya mpunga na bustani zao ambazo hulima majira yote.


Kikundi kimojawapo cha kijiji cha Gumali kinachojishughulisha na kulima bustani.

Tumeweza kuisimamia vizuri serikali na hivyo kuwa na bei inayomlipa mkulima kwenye zao la pamba. Mfano mwaka wa fedha 2014/15 bei ya pamba ilikuwa Tshs 800, mwaka wa fedha 2015/16 bei ya pamba ilipanda kufikia Tshs 1000, mwaka wa fedha 2016/17 bei ilikuwa 1200, mwaka wa 2017/18 bei ilikuwa Tshs 1100, na mwaka wa fedha 2018/19 bei ni Tshs 1200. Kutoshuka kwa bei ya pamba ni matokeo ya usimamizi mzuri wa bunge kwa serikali kuhakikisha kwamba wakulima hawapunjwi mazao yao wanayozalisha kwa jasho kubwa. Matokeo yake uzalishaji katika zao la pamba umeongezeka na mwaka huu wa 2019 uzalishaji umeongezeka Zaidi.

6.      VIWANDA
Katika kutimiza adhima ya Tanzania ya viwanda ifikapo 2025, jimbo limewezeshwa kuanzisha viwanda viwili, kimoja cha kuongeza viini lishe kwenye unga wa viazi ambacho kimejengwa kijiji cha Njiapanda.

7.      MINADA NA MASOKO.

Jimbo lina minada ya ng’ombe mikubwa 2 panapouzwa na kununua nafaka, mifugo, nguo, nk. Minada hiyo ni Malampaka na Jija. Mwaka 2015 mnada wa Jija ulikuwa na changamoto kiasi kwamba mnada haukuwa unafanya kazi kwa sababu ya kuzidiwa kete na halmashauri ya wilaya ya Kwimba walipoanzisha mnada wa Maligisu kinyemela. Mbunge kwa kushirikiana na halmashauri ya wilaya ya Maswa alifanya juu chini kuufufua mnada huu ikiwa ni pamoja na kuwasiliana na wizara ya mifugo makao makuu na hatimaye mnada huo ulianza tena kufanya kazi mwaka 2017. Katika minada hii pia kulikuwa na kero mbalimbali kama vile ushuru uliokuwa ukijulikana kama makanyagio. Ushuru huu wa makanyagio umefutwa na serikali kwa kuzingatia ushauri uliotolewa na mbunge akishirikiana na wabunge wengine wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

8.      MICHEZO NA BURUDANI.
Kwa upande wa michezo na burudani, tumejitahidi sana kuwaunganisha vijana walioko mashuleni na wasio shuleni kwa njia ya michezo na burudani. Maeneo mengi tumeweza kutoa mipira ya mguu, mipira ya pete, jezi na kugharamia kuweka magoli kwenye baadhi ya viwanja vya michezo hasa vya mpira wa miguu shuleni.


Mheshimiwa mbunge akitoa mpira kwa moja ya shule ya msingi jimboni.


Mheshimiwa mbunge alipokuwa mgeni rasmi kwenye mashindano ya ligi ya mkoa wa Simiyu. Mashindano yalifanyika wilaya ya Maswa uwanja wa CCM.


Mheshimiwa mbunge wakati alipotoa zawadi kwa washindi ligi ya mpira wa miguu iliyofanyika shishiyu sekondari.


MWISHO.

Comments